Na Gideon Gregory – Dodoma.
Zaidi ya Milioni 500 zitagawiwa kwa wasanii ambazo ni asilimia 6 ya tozo ya hakimiliki na kiasi cha zaidi ya Milioni 84 kinaenda katika Mfuko wa Sanaa na Utamaduni.
Hayo yameelezwa Jijini Dodoma na Katibu Mtendaji wa Ofisi ya Hakimiliki Tanzania (COSOTA), Doreen Sinare wakati akizungumza na Waandishi wa Habari wakati juu ya mafanikio na mwelekeo wao katika kipindi Cha miaka minne ya Serikali ya awamu ya Sita.
Aidha Bi.Sinare amesema katika kipindi hicho kamati maalumu ya Usajili ndani ya COSOTA inayojihusisha na masuala ya usajili, imefanikiwa kutoa mafunzo na ufafanuzi kuhusiana na hakimiliki kwenye kazi zilizopokelewa katika kipindi hicho kwa idadi ya wabunifu 167.

Hata hivyo amesema katika kipindi cha Miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan COSOTA imefanikiwa kupokea jumla ya migogoro 136.
Akigusia suala la migogoro, amesema Migogoro 118 imetatuliwa, migogoro 10 haijafanyiwa kazi bado na Migogoro 8 bado inafanyiwa kazi.
Pamoja na kushughulikia migogoro, COSOTA pia imekuwa ikihusika katika kesi kumi za hakimiliki, ikiwa ni hatua muhimu katika kulinda haki za wabunifu dhidi ya uharamia na matumizi yasiyoidhinishwa ya kazi zao.
Bi. Sinare amesema kupitia Tozo ya Hakimiliki , COSOTA imekusanya jumla ya shilingi bilioni 1.42 kuanzia Septemba, 2023 hadi Februari, 2025 ambapo Ofisi imefanikiwa kupokea fedha za tozo ya hakimiliki za mwaka wa fedha 2023/2024 kutoka Wizara ya Fedha zaidi ya shilingi milioni 840.
Kwa mujibu wa Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki pamoja na Mabadiliko Sheria ya Fedha Na. 5 ya mwaka 2022, kiasi cha tozo ya Hakimiliki kilichokusanywa ndani ya mwaka husika hugawanywa kwa makundi manne katika asilimia.
Ambapo COSOTA inachukua 20%, Mfuko wa Utamaduni 10%, Mfuko Mkuu wa Serikali 10%, na Kampuni za kukusanya na kugawa mirabaha (CMOs) kwa ajili ya wasanii, waandishi na wamiliki wengine wa hakimiliki 60%.
Aidha, kwa mwaka 2021 – 2025 COSOTA imefanikiwa kufanya migao miwili kama alivyoahidi Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan alipolihutubia bunge mwaka 2021 ambapo alisisitiza katika kipindi cha uongozi wake, serikali itahakikisha wabunifu wote wananufaika zaidi na kazi zao.
Ambapo Mgao wa kwanza ambao ulikuwa ni mgao wa ishirini na tatu ulifanyika tarehe 28/01/2022 na ulikuwa wa kiasi cha Tshs. Tshs. 312,290,259,000, ambapo Wasani 1,123 walinufaika, na ulitokana na matumizi ya kazi 5,924 za muziki ambazo zilitumika katika vituo 11 vya redio, ikiwemo redio katika ngazi ya kitaifa, Mkoa, wilaya, kijamii na za kidini
Mgao wa pili katika kipindi cha serikali ya awamu ya sita ulifanyika tarehe 21/07/2023 na ulikuwa ni mgao wa ishirini na nne wa mirabaha kwa kazi za muziki na COSOTA iligawa kiasi cha Tshs. 396,947,743.20 na wasanii wa muziki 8,165 walinufaika kupitia kazi zao 61,490.