Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema Kampeni ya Kitaifa ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia ni ubunifu wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan uliolenga kuongeza wigo wa upatikanaji haki kwa wananchi wasio na uwezo wa kumudu gharama za huduma za kisheria.
Amesema kuwa kupitia kampeni hiyo ambayo inatolewa bure mpaka sasa imefanikiwa kuwafikia zaidi ya wananchi milioni moja wakiwemo wanawake 681,326 na wanaume 691,773 katika mikoa 19 nchini.
Amesema hayo hii leo Jumatano Februari 19, 2025 wakati alipozindua kampeni ya Kitaifa ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia katika mkoa wa Lindi, kwenye viwanja vya Madini, Ruangwa Mkoani Lindi.

“Mheshimiwa Dkt. Samia alijifunza shida, kero na changamoto wanazopata watanzania na hasa wale ambao hawana uwezo wa kulipia gharama za huduma za kisheria, aliguswa na akaamua kuanzisha kampeni hii na kuikabidhi Wizara ya Katiba na Sheria isimamie.”
Ameongeza kuwa kupitia kampeni hii migogoro mbalimbali ya ardhi, ndoa, mirathi imetatuliwa. Ni ukweli isiopingika kuwa, jamii nyingi zimekuwa na changamoto kuhusu mirathi ambazo zinachangia kuondoa amani miongoni mwa wanandugu kwa kugombania mali.”

Aidha, Majaliwa ametoa wito kwa wakuu wa wilaya nchini kuweka mpango wa kufanya ziara kwenye maeneo yao wakiwa na wanasheria ili kusikiliza na kutatua kero za kisheria za wananchi badala ya kusubiri viongozi wa kitaifa.
“Watanzania wanahitaji huduma ya Serikali hii na Serikali imefanya kazi kubwa sana kwenye nchi hii na bado tumeahidi kuwatumikia.”

Majaliwa amesema kuwa, pamoja na kampeni hiyo, Rais Dkt. Samia amefanya mageuzi makubwa na kuweka kipaumbele katika kutatua changamoto zilizopo sekta ya huduma za sheria nchini.
Pia, Majaliwa ameiagiza Wizara ya Katiba na Sheria kupitia Ofisi ya Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini RITA kuongeza kasi ya utoaji elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa kuandika na kutunza wosia na kugawa mirathi kwa mujibu wa sheria ili kupunguza migogoro miongoni mwa wanafamilia.

Naye, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Prof. Palamagamba Kabudi amesema kuwa kampeni ya msaada wa kisheria ya mama Samia unasifa nne ambazo ni umuhimu wake kwa jamii, umaalum wake ni kwasababu inatelekeza maelekezo ya Rais Dkt. Samia, umahususi wake imeasisiwa na Rais Dkt. Samia “ukipekee wake ni kwasabau inatekeleza falsafa ya 4R.”
Kwa Upande wake Naibu Waziri Katiba na Sheria Jumanne Sagini amesema kuwa Wizara ya Katiba na Sheria inaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuhakikisha wananchi wanaifikia haki kwa wakati na kwa ufanisi.

Amesema kuwa ili kuhakikisha lengo hilo linawezekana, Wizara imeendela kutoa mafunzo kwa wasaidizi wa kisheria na kujenga uwezo kwa watoa huduma za msaada wa kisheria ili kuendelea kusogeza zaidi huduma hizo karibu na wananchi.
“Mwezi Desemba, 2024, Wizara iliingia makubaliano na Chama cha Wanasheria Tanganyika kwa lengo la kuimarisha zaidi huduma za uwakili kwa wananchi wasiokuwa na uwezo wa kumudu gharama za mawakili.”