WAZAZI ENDELEZENI VIPAJI VYA WATOTO KWA KUWASOMESHA – DC MASINDI

Na Eunice Kanumba – Shinyanga.

Mkuu wa Wilaya ya Kishapu Mkoani Shinyanga, Peter Masindi amewataka wazazi kuwasomesha watoto wao na kuwaendeleza kwenye vipaji mbalimbali hususan wale waliofeli masomo na kuwataka kuwekeza zaidi kwenye malezi bora yenye kufuata maadili ya Kitanzania, huku akiahidi kuendelea kutatua changamoto za Wananchi

Masindi ametoa rai hiyo wakati akisikiliza na kutatua kero za wananchi wa Kata za Mwataga, Kishapu na Uchunga kwa kufanya mikutano ya hadhara katika maeneo hayo.

Amesema, “Ndugu zangu wananchi niwapongeze kwa kuendelea kuiamini serikali ya awamu ya sita na pia napenda kuhamasisha kuendelea kufanya kazi kwa bidii, kuepuka mikusanyiko isiyo na tija na kuwekeza zaidi katika familia zenu hususa ni katika maendeleo ya wanawake na watoto.”

Akijibu maswali ya Sekta ya Elimu, Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Kishapu, David Mashauri amesema Halmashauri imeanza kupokea fedha kwa ajili ya kujenga Shule shikizi katika maeneo yenye changamoto ya watoto kutembea umbali mrefu, huku Kitongoji cha Lubaga kilichoko Kata ya kishapu kikiwa ni miongoni mwa wanufaika.

Amesema, Shule ya Msingi Bukingwa-Mandenge na Bulima tayari zimepangiwa fedha kwa ujenzi wa madarasa, huku nyumba ya Walimu Shule ya Msingi Lubaga ikiwa kwenye bajeti ya mwaka wa fedha 2025/2026 wanasubiria fedha ili kuboresha jengo hilo.

Kwa upande wake Meneja wa RUWASA Wilayani humo, Dickson Kamazima amesema Serikali inaendelea kusogeza huduma ya maji safi kwa wananchi ambapo kwa Kitongoji cha Mwataga utekelezaji umefikia asilimia 95, na maeneo mengine yatapatiwa huduma kupitia maji ya Ziwa Viktoria na visima vinavyochimbwa kisasa.

Aidha, amesema wiki ya kwanza ya Septemba watafanya uthamini katika Kitongoji cha Migunga ili kusogeza huduma hiyo kupitia kwenye bomba kubwa la maji linaloelekea Kata ya Lagana, huku Kitongoji cha Mwanulu kikiwa kwenye mpango wa kusogezewa huduma pia baada ya kupokea fedha kutoka serikalini.

Kuhusu suala la umeme, Mwakilishi wa Meneja wa TANESCO Wilayani humo, Gidion Kanan amesema Serikali inaendelea kusambaza Nishati hiyo kwenye Vijiji na vitongoji kote Wilayani humo, huku akitoa wito kwa Wananchi kuendelea kulinda miundo mbinu ya umeme.

Miongoni mwa changamoto zilizowasilishwa katika Mkutano wa DC Masindi ni pamoja huduma ya maji safi, upatikanaji wa umeme, uboreshaji wa barabara na miundombinu ya mawasiliano katika kata ya Uchunga, huduma za afya katika Zahanati ya Lubaga na ujenzi wa nyumba ya walimu katika Shule ya Msingi Lubaga katika kata ya Kishapu.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *