Na Eunice Kanumba – Shinyanga.
Vituo vya Kulea Watoto wadogo mchana Mkoani Shinyanga, vimetakiwa kuwa na usajili na kufuata utaratibu uliowekwa na mamlaka, ili kuweza kuwalinda Watoto kwa mujibu wa sheria ya watoto namba 21 ya mwaka 2009.
Agizo hilo, limetolewa na Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga, David Lyamongi wakati akifungua kikao kilicho husisha wamiliki wa Vituo vya Kulea Watoto mchana katika kuangalia hali ya utekelezaji wa Programu Jumuishi ya Taifa ya Maendeleo ya Awali ya Mtoto (PJT-MMMAM) kuanzia mwezi Januari hadi Juni mwaka 2025.
Aidha, amewapongeza wamiliki wote wa vituo vya kulea Watoto wadogo mchana pamoja na makao ya Watoto kwa kazi nzuri ambayo wamekuwa wakiifanya ya utoaji wa huduma hiyo.

Akiwasilisha mada juu ya vitendo vya kuzia na kupambana na vitendo vya rushwa katika kikao hicho, Afisa kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Shinyanga, Mohamed Doo amesema Serikali itaendelea kuimarisha mifumo mizuri na kuziba mianya ya utoaji rushwa kwa kuhakikisha unakuwepo uimara thabiti.
Doo amesema Programu Jumuishi ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto (PJT-MMMAM) ni nzuri na imewaleta wadau pamoja lakini suala la kukemea vitendo vya rushwa watoto wadogo waanze kufundishwa kupitia nyimbo nzuri zenye maudhui ya kupinga.

Amesema, watu wamejenga desturi ya kuhalalisha rushwa, ili apate kitu kwa urahisi nakujaribu kutumia njia ya mkato na ushawishi kwa lengonla kupata kile walichokusudia na jamii kukubali pasipo kutoa taarifa kwenye mamlaka.
“Tumekuwa tukishtaki watuhumiwa wanaoendesha vitendo vya rushwa kwa watumishi wa taasisi za serikali na taasisi binafsi kwani watu wanajihusisha wanapobainika wanachukuliwa hatua,” amesema Doo.

Ameongeza kuwa, “sisi tunapokea taarifa nyingi kutoka maeneo tofauti tofauti kwani zipo baadhi ya familia zinazotoa hongo ili watoto wao waliopo kwenye vituo walelewe vizuri zaidi kuliko wengine kwa kufanya hivyo hutamjenga itaonyesha kubaguliwa au kujibagua kwa mtoto mwenyewe nakujiona mnyonge.”
Aidha, alisema zipo rushwa zinazotolewa kwenye vituo kama misaada hasa kwa Watoto wanaolelewa kwenye makao na vituo kwa malengo yao na mbinu hizo zimekuwa zikitumika kuleta maadili yasiyofaa kwa watoto.


