Na Frank Aman – Geita.
Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Taifa Mkoa wa Geita, Evarist Gervas amesema Vijana wametakiwa kujitokeza katika Uchaguzi Mkuu wa Mwaka huu pindi wakati utakapofika wagombee nafasi za udiwani na ubunge badala kuwa wasindikizaji.
MNEC Gervas amesema hayo wakati wa ufunguzi wa semina ya Viongozi wa Umoja wa Vijana wa CCM Mkoa wa Geita iliyofanyika Mjini Geita.
Akizungumza katika Mkutano huo Gervas amesema kuqa anaamini mkoa wa Geita unao vijana wenye weledi wenye sifa ambao wanastahili kwenda kuomba nafasi wakati ukifika lakini amewasihi wasiishie tuu kwenye nafasi ya Udiwani waende wakachukue nafasi za ubunge maana nafasi ya ubunge haina mwenyewe ni mtu yeyote mwenye sifa kuanzia umri wa miaka 18 na kuendelea.

Ameongeza kuwa anavyowaangalia UVCCM Geita anawaona wanazo sifa na umri unaostaili ambapo ameeleza tatizo lao wamejipa nafasi ya kuwa wapambe wa wagombea.
Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Geita,Manjale Magambo amesema vijana wapo tayari kwa ajili ya kujitokeza kugombea nafasi ya udiwani na ubunge katika uchaguzi mkuu ujao na ametoa rai kwa vijana kuendelea kusemea utekelezaji wa miradi iliyotekelezwa na serikali.
Manjale pia amewataka Vijana kuwa mstari wa mbele kugombea nafasi mbalimbali za Uongozi sambamba na kuwaonya wanaotaka kuvuruga uchaguzi mkuu kuacha hila zao kwani Serikali ipo makini katika suala hilo .
Mwenyekiti wa Uvccm Wilaya ya Geita, Naomi Fujo amesema kwa uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka jana zaidi ya asilimia 40 ya vijana wamechaguliwa nafasi mbali mbali katika uchaguzi wa serikali za mitaa na amesema watajitahidi kwa uchaguzi mkuu ujao kuwahamasisha vijana kujitokeza.


