Mkurugenzi wa Bodi ya Sukari nchini, Profesa Kenneth Bengesi amesema kuwa Serikali imetoa vibali vya kuagiza sukari tani 50,000 kutoka nje ya nchi ili kukabiliana na uhaba wa bidhaa hiyo ambapo itaanza kuwasili mwezi huu.
Kwa sasa Sukari imekuwa adimu nchini na imesababisha kupanda bei na kufikia kati ya TSh 3,200 mpaka TSh 4,000 kutoka TSh 2,500 hadi Tsh 3,200.
Upungufu wa sukari umetokana na upungufu wa bidhaa hiyo kwenye maghala kulikosababishwa na viwanda kusimamisha uzalishaji kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha.
Bengesi amesema baada ya viwanda kusimama uzalishaji, sukari iliyokuwa inatumika ni iliyozalishwa mwezi Mei 2023 na hivyo kusimama kwa uzalishaji kulimaanisha sukari iliyokuwepo kwenye maghala kupungua kwa kiasi kikubwa hali iliyofanya wafanyabiashara wasio waaminifu kutumia mwanya huo kupandisha bei.