Na Daniel Gahu – Katavi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika Mkoa wa Katavi, Shaban Juma ameongoza timu ya Watalaam wa Halmashauri katika kukagua miradi baadhi itakayopitiwa na mwenge wa uhuru ifikapo Septemba 23, 2025.
Katika ziara hiyo, ameagiza ukamilishwaji wa miradi kwa wakati, ikiwemo kuwaomba wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika kujitokeza kwa wingi kuupokea mwenge, ambao utapita kwenye maeneo yao kutembelea, kuzindua miradi na kuweka mawe ya msingi kwenye miradi mbalimbali.

Katika ziara hiyo Mkurugenzi Mtendaji aliambatana na watalaam kutoka idara ya ujenzi na miundombinu, idara ya mipango, Mratibu wa Mwenge Wilaya ya Tanganyika, Mtendaji wa Kata ya Tongwe, na wajumbe mbalimbali wa kamati za ujenzi kwenye miradi hiyo.
Miradi iliyotembelewa na ziara hii ni Zahanati ya Kijiji cha Vikonge, Bweni la wasichana shule ya Sekondari Majalila, aidha mbali na miradi hii timu ya Watalaam iliweza kutembelea na kuona hali ya ujenzi wa uzio kwenye nyumba za wakuu wa Idara wa Halmashauri.



