Serikali imeendelea kufanya maboresho katika sekta ya afya kwa kuongeza kiwango cha upatikanaji wa dawa na vifaa tiba ambapo imetoa magari sita ya kubebea wagonjwa katika Halmashauri zote za Mkoa wa Shinyanga na vipimo vya kisasa vya kugundua ugonjwa wa saratani ukiwa katika hatua ya awali katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga iliyopo katika kata ya Mwawaza.
Akithibisha kupokea magari na vifaa hivyo Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Christina Mndeme amesema tayari amekabidhiwa na Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan na atakabidhi vifaa hivyo katika Halmashauri zote za mkoa wa Shinyanga huku akiwataka watumishi kuyatunza magari na vifaa tiba hivyo ili viweze kuhudumia na vizazi vijavyo.
Aidha Mndeme amewataka madaktari na wauguzi katika Hospital ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga kuzuia suala la upotevu na wizi wa madawa hospitalini hapo huku akiagiza hatua za haraka zichukuliwe pindi inapobainika kuna mtu ameiba dawa na vifaa tiba kwani dawa hizo zinaletwa kwa ajili ya wananchi.
Sekta ya afya imeendelea kuboreshwa na Serikali ya Awamu ya sita na katika mwaka wa fedha 2022/2023 serikali ilitenga zaidi ya shilingi bilioni 200 kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba huku Bilioni 74.3 zikiwa tayari zimetolewa katika kumaliza changamoto ya upungufu wa dawa na vifaa tiba hasa katika maeneo ya vijijini.