Categories

Do you have a Story?

Call us on 0677 644 444 to submit your news story or incident report!

Noti Bandia,Pisto,Watu 25 Mikononi Mwa Jeshi la Polisi Shinyanga

Na Ibrahim Rojala,Shinyanga

Jeshi la Polisi Mkoani Shinyanga limefanikiwa kukamata noti bandia 42 zenye thamani ya shilingi 420,000 na kuwatahadharisha wananchi hasa wakulima wanaouza mazao kuepuka kupokea fedha nyingi nyakati za usiku kutokana na uwepo wa wimbi la noti bandia.

Rai hiyo imetolewa na Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP, Kennedy Mgani wakati akitoa taarifa kwa vyombo vya habari leo Jumatano Juni 26,2024 ambapo amesema Jeshi la Polisi mkoa wa Shinyanga katika kipindi cha mwezi mmoja kuanzia tarehe 26/05/2024 hadi 25/06/2024 kwa kushirikiana na jamii limeendelea kuimarisha hali ya usalama wa raia na mali zao kwa kukabiliana na vitendo mbalimbali vya kihalifu na wahalifu kupitia misako na doria katika maeneo mbalimbali ya mkoa wa Shinyanga.

“Hizi fedha zilizokamatwa kama zingekuwa ni halali zingekuwa na thamani ya shilingi 420,000/=, haziihitaji hata utaalaamu kwa tupeleke Benki Kuu lakini tutapeleka kwa ajili ya hatua zingine ili kuthibitisha. Mtanzania aliyezoea kutumia fedha hata kwa macho tu anaona kabisa hizi ni noti bandia.

Katika kipindi hiki cha mavuno ili kukabiliana na matukio ya uhalifu mbalimbali ni pamoja na hizi fedha bandia zimekamatwa wakati zikiwa zinatakiwa kuingia kwenye mzunguko wa ununuzi wa mazao ya wakulima wetu, tunaendelea kutoa elimu kwa wananchi wawe makini kupokea fedha nyingi hasa nyakati za usiku, kwani wimbi la noti bandia lipo, watoe ushirikiano pindi wanapotilia mashaka kwamba mbona hizi noti hazipo katika uhalali”,amesema Kamanda Mgani.

Ameongeza kuwa kutokana na misako na doria zilizofanywa na Jeshi la Polisi pia vielelezo mbalimbali vilikamatwa katika matukio ya kihalifu ikiwemo Silaha moja aina ya Browning Pistol ambayo ilitumika katika tukio la unyang’anyi huko Halmashauri ya wilaya ya Msalala, Mabomba 10 ya maji, pamoja na Pikipiki 05, vitu mbalimbali vinavyotumika katika masuala ya ramli chonganishi, mtambo 01 wa kutengenezea Pombe haramu ya moshi, TV 01, meza 02, kabati 01 la kuwekea TV, milango 02 na madirisha 04 ya chuma.

Mgani amesema jumla ya watuhumiwa 25 wanashikiliwa katika vituo mbalimbali vya Polisi kuhusiana na tuhuma za kufanya uhalifu huku wakisubiri kufikishwa mahakamani na wengine wakipewa dhamana.

Amebainisha kuwa katika kipindi hicho cha mwezi mmoja, jumla ya kesi 08 zilihukumiwa mahakamani kwa mafanikio kama ifuatavyo. Kesi 02 za kulawiti zilihukumiwa kifungo cha maisha jela, Kesi 01 ya kujeruhi ilihukumiwa kifungo cha miaka 03, Kesi 02 za wizi zilihukumiwa kulipa fine ya Tsh, 300,000/, Kesi 01 ya kupatikana na Bangi ilihukumiwa kifungo cha nje miezi 12, na kesi moja ya kubaka ilihukumiwa kifungo cha nje miezi 06, mtuhumiwa alikuwa na umri wa miaka 17.

Kwa upande wa usalama barabarani jumla ya makosa 3438 ya magari yalikamatwa ma makosa ya pikipiki na Bajaji yalikuwa ni 1,496 huku dereva 01 wa magari akifungiwa leseni yake kwa kukiuka sheria za usalama barabarani”,ameeleza.

“Jeshi la Polisi mkoa wa Shinyanga linatoa wito kwa wananchi wote kuendelea kuzingatia sheria za nchi ili kuweza kushughulika na kazi zingine za kiuchumi ambazo ni halali”,amesema.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *