Katika hali isiyokuwa ya kawaida mtoto mwenye umri wa miaka 12 ambaye alikuwa akisoma darasa la nne katika shule ya msingi Ndembezi- Manispaa ya Shinyanga amekutwa amejinyonga kwa kutumia mtandio katika chumba alichokuwa akilala huku chanzo kikitajwa kuwa ni kufokewa na mama yake mdogo baada ya kumaliza maji aliyokuwa akioga na wadogo zake kisha kuambiwa akachote maji mengine.

Mjumbe wa serikali ya mtaa wa Ndembezi Rubeni Doto akizungumza na Jambo Fm kuhusiana na tukio hilo amesema wamesikitishwa na tukio hilo kwani marehemu alikuwa ni mtoto mwenye ndoto nyingi za kufanikisha maisha yake.
Kwa upande wake mama mdogo wa mtoto huyo Esta Joeli ambaye ndiyo alikuwa akiishi naye amekiri kumfokea mtoto huyo baada ya kutumia maji yote aliyokuwa anatakiwa kutumia na wadogo zake huku akimtaka akachote maji mengine ambapo mtoto huyo hakujibu kitu badala yake alikwenda chumbani kwake na baaday ya muda mfupi walipoingia walimkuta amejinyonga.
Jambo Fm imezungumza na mashuhuda wa tukio hilo ambapo wamesema mtoto huyo alikuwa akiishi vizuri na mama yake mdogo na wakati mwingine mtoto huyo alipokosea alikuwa akionywa kama watoto wengine hivyo wanashangaa ni kwa nini mtoto huyo amechukua hatua hiyo.
Kamanda wa jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga Acp Janethi Magomi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo huku akisema jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi ili kubaini kama ni kweli mtoto huyo amejinyonga au amenyongwa na uchunguzi ukikamilika atatoa taarifa kwa vyombo vya habari.