Jumla ya mifugo wapatao 298,024 wakiwemo Ng’ombe,Kondoo na Mbuzi wanatarajiwa kupatiwa chanjo ya homa ya mapafu katika halmashauri ya Ushetu wilani Kahama mkoani Shiyanga.
Hayo yamebainishwa na Mkuu wa Divisheni ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Deus Kakulima wakati akizindua chanjo hiyo katika kijiji cha Chambo kilichopo kata ya Chambo Halmashauri ya Ushetu.
Amesema, zoezi hilo kwa Halmashauri ya Ushetu limeanza Septemba 1, 2025 na litatamatika Septemba 20, 2025 likitarajiwa kufika katika kata zote 20.

“Zoezi hili tumelianza leo Septemba 1 na tunatarajia kufika katika kata zote 20 vijiji 112 na tutahitimisha Septemba 20 mwaka huu ambapo jumla ya mifugo 298,024 wakiwemo Kondoo mbuzi na Ngombe wanatarajia kuchanjwa chanjo ya homa ya Mapafu” Amesema Kakulima.
Aidha, ametoa wito kwa wafugaji wote kupeleka mifugo yao kupatiwa chanjo hiyo muhimu ambayo inatolewa kwa kwa ruzuku ya serikali na mfugaji atachangia kiasi kidogo kwa kila mfugo.
“Nitoe rai kwa wafugaji wote leteni mifugo yenu katika maeneo ya kuchanjia ili kufanikisha chanjo hii muhimu kwa mifugo yetu ambayo huduma hii tunaitoa kwa fedha za ruzuku ya serikali na mfugaji atatakiwa kuchangia shilingi 500 kwa kila ng’ombe na shilingi 300 kwa ng’ombe na kondoo,” ameongezea Kakulima.

Akiongea kwa niaba ya wafugaji wenzake, Donald Mtogwa wa kijiji cha Chambo ameishukru Serikali kwa kuwaletea huduma hiyo muhimu kwani awali walikuwa wanatumia fedha nyingi kununua chanjo mitaani.
“Sisi wafugaji, tunasema Asante sana kwa Serikali yetu kwa kutuletea huduma hii muhimu, kwani mara kadhaa tumekuwa tukipatwa na kadhia hii ya kupoteza mifugo yetu,lakini wakati mwingine tumekuwa tukinunua chanjo hizo kwa bei kubwa mitaani lakini sasa mifugo yetu itastawi sana na itakuwa salama,” amesema Mtogwa.
Zoezi hilo linalenga kupunguza vifo vya mifugo kwa wafugaji kwenye Halmashauri hiyo,kutokana na matukio mengi ya wafugaji kupoteza mifugo yao kutokana na ugonjwa wa homa ya mapafu,Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu ina jumla ya Ng’omb 190,000, Mbuzi 84,688 na Kondoo 24,336.


