Na Eunice Kanumba – Shinyanga.
Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, imevuka lengo la ukusanyaji mapato ya ndani katika Mwaka wa fedha 2024/2025 na kukusanya sh.bilioni 6.5 dhidi ya lengo la Sh.bilioni 6.4
Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi wa halimashauri ya Manispaa ya Shinyanga mwalimu Alexius Kagunze, wakati akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake,kuhusiana na mafanikio hayo.
Amesema katika mwaka huo wa fedha ambao umeisha ,walipanga kukusanya mapato ya ndani kiasi cha sh.bilioni 6.4, lakini hadi kufikia Juni 27,2025, wamevuka lengo na kukusanya sh.bilioni 6.5 sawa na asilimia 102.

“Tuna washukuru wananchi wa Shinyanga,kwa ulipaji wa mapato na ushuru kwa hiari yao, na kufanikisha kuvuka lengo la ukusanyaji mapato kwa mwaka wa fedha 2024/2025 na kupata sh.bilioni 6.5,”amesema Kagunze.
Kagunze ametaja sababu zilizosababisha kuvuka lengo hilo,kuwa ni pamoja na kutoa elimu kwa wananchi na wafanyabiashara juu ya umuhimu wa ulipaji wa mapato, pamoja na watumishi kujituma kukusanya mapato yao kwa uaminifu mkubwa.
Aidha,amesema fedha hizo zitatumika katika matumizi mbalimbali ya miradi ya maendeleo katika manispaa hiyo ikiwemo ujenzi wa madarasa,matundo ya vyoo,umaliziaji ujenzi maboma ya Zahanati,hususani boma lililopo Mwamagunguli kwani limekuwa limekuwa ni la muda murefu sana,pamoja na ugharimiaji wa shughuli za uendeshaji wa Manispaa.


