Na Gideon Gregory – Dodoma.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika kilele cha Maadhimisho ya wiki ya anuani za makazi nchini, yatakayohitimishwa Februari 8, 2025.
Hayo yamesemwa Jijini Dodoma na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Jerry William Silaa wakati akifungua maadhimisho hayo yenye kauli mbiu inayosema “Tambua na tumia anwani za makazi kurahisisha utoaji na upokeaji wa huduma.”

Amesema mfumo wa anwani za makazi ni muunganiko wa taarifa na miundombinu ambayo kwa pamoja inatambulisha anwani halisi ya kitu au mtu alipo ili kurahisisha utoaji na upokeaji wa huduma hivyo kwa kutambua hilo serikali kupitia wizara ya mawasiliano na teknolojia ya habari kwa kushirikiana na wadau wengine hususan Ofisi ya Rais-TAMISEMI na wizara ya ardhi, nyumba na maendeleo ya makazi inaratibu utekelezaji wa mfumo wa anwani za makazi nchini.

“Dhamira ya serikali ni kuhakikisha kuwa kila nyumba, jengo, kiwanja, huduma, ofisi ama eneo la biashara linatambulika kwa anwani ya makazi, anwani ya Makazi inaundwa na namba ya anwani maarufu kama namba ya nyumba, Jina la barabara au mtaa na Postikodi,”amesema.
Aidha amesema utekelezaji wa mfumo wa anwani za makazi ulianza mwaka 2010 na kwa mujibu wa mpango wa utekelezaji ulitakiwa ukamilike mwaka 2015 hata hivyo, utekelezaji wake ulikuwa wa kasi ndogo ukilinganisha na matarijio, hali iliyosababisha kuanzishwa kwa operesheni maalumu iliyojulikana kama operesheni anwani za makazi ambayo ilizinduliwa na Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Februari, 8, 2022.

Sambamba na hayo amesema kuwa utekelezaji wa mfumo wa anwani za makazi ni endelevu kwa sababu ya mabadiliko ya makazi, wakazi, na huduma hivyo shughuli mbalimbali za mfumo zinaendelea kutekelezwa ikiwemo kukusanya, kuhakiki na kuhuisha taarifa za anwani za makazi, kuboresha utendaji kazi wa Mfumo wa NaPA, kutoa elimu kwa umma na kuhamasisha utekelezaji, uendelezaji na matumizi ya mfumo wa anwani za makazi.

Kwa upande wake Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Dkt. Festo Dugange, amesema uwepo wa huduma za anwani za makazi zimesaidia kurahisisha kazi kufanyika kwa njia ya tehama na uboreshaji utoaji wa huduma za jamii.
“Kwa upande wa Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na OR- TAMISEMI tumekubaliana kuendelea kutoa mafunzo ya mfumo wa anwani za makazi kwa waratibu wa mikoa na Hhalmashauri.”

Dugange amesema kuwa “mafunzo mengine yatakuwa yanatolewa kwa njia ya TEHAMA (online training), hivyo Makatibu Tawala wa Mikoa na wakurugenzi wa halmashauri muwaruhusu, muwahamasishe na muwahimize waratibu wenu kushiriki mafunzo haya kwa kadri ratiba zitakazoandaliwa”.


