Kila la kheri Stars leo

Timu ya soka ya Tanzania, Taifa Stars leo Alhamis (Septemba 07) itakuwa na kazi moja tu ya kusaka angalau pointi moja ili kuweka rekodi ya kucheza Fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON) kwa mara ya tatu katika historia ya nchi itakaposhuka dimbani kucheza dhidi ya Algeria, huku Serikali ikiitakia kila la kheri.

Stars itashuka kwenye Uwanja wa Mei 19 uliopo kwenye mji wa Annaba Kaskazini mwa nchi hiyo majira ya saa 4:00 kwa saa za Afrika Mashariki, ikijaribu kurudia ilichokifanya mwaka 1979 na 2018 ilipofuzu kucheza AFCON ambazo Fainali zake zilichezwa 1980 nchini Nigeria na 2019 nchini Misri.

Stars inayohitaji ushindi au sare ipo kwenye Kundi F, ambalo linahitaji timu moja kuungana na Algeria ambayo tayari imefuzu kucheza Fainali hizo.

Msimamo wa kundi hilo kabla ya michezo ya leo, Algeria anaongoza akiwa na pointi 15 akifuatiwa na Taifa Stars wenye pointi saba huku Uganda wakishika nafasi ya tatu wakiwa na pointi nne huku Niger ikiburuza mkia.

Kutokana na msimamo huo, Stars hata ikipata sare itakuwa imefuzu moja kwa moja Fainali hizo zitakazochezwa Ivory Coast hata kama Uganda itafanikiwa kuifunga Niger.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *