KIEMBA AMTETEA CHASAMBI AKIMNYOOSHEA KIDOLE CAMARA

Mchezaji nyota wa mpira wa miguu wa zamani ambaye amegeukia uchambuzi wa soka, Amri Kiemba amemtetea winga wa Simba SC, Ladark Chasambi ambaye alijifunga goli katika mchezo wao na Fountain Gate FC.

Kupitia ukurasa wake wa mtandao wa Kijamii, Kiemba amesema ni mambo mawili yakitokea mchambuzi atamlaumu Ladarck Chasambi ambayo ni kama umesahau na kama haufahamu moja ya msingi wa mpira wa miguu ambao ni kuutunza mpira, na hasa kwa kuutoa mpira sehemu yenye vurugu na kuupeleka palipotulia.

“Kama unafahamu kanuni au principle hii hauwezi kumlaumu Chasambi kupita kiasi, angalia hao wachezaji wa FG niliowawekea mishale, wote wanatoa shinikizo kwa Chasambi, wamefunga njia karibu pande zote na kuacha chaguo moja kubwa la kucheza na golikipa wake,” alifafanua Kiemba.

Kiemba anasema, “na golikipa Camara alitambua kuwa Chasambi ana chaguo moja tu la kumrudishia yeye mpira na Camara akaonesha utayari wa kuucheza mpira, wanaocheza mpira na walimu wataungana na mimi kuwa mpira una lugha yake na Camara aliitumia kuonesha utayari.”

Hata hivyo, Kiemba anaelezea kwamba “kitu pekee ninachoweza kumkumbusha Chasambi ni kuwa wazo lake lilikua sahihi lakini mguso wake kwa mpira ulikuwa mzito na kuufanya mpira uende mbali na kwa kasi zaidi wenzetu wanasema (heavy touch).”

“Ninachoweza kumkumbusha Camara ni alitakiwa kusogea kushoto kwa haraka kukutana na boli, ni kama alichelewa kidogo kushiriki mchezo, na misstiming kwa Camara imewai kutokea pia katika mechi ambayo Coastal Union wanasawazisha dhidi ya Simba SC,” alimaliza kuandika Kiemba.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *