Imeelezwa kuwa watu wanaojihusisha na ubebaji wa vyuma vizito pamoja na mizigo iliyopitiliza wapo hatarini kuugua ugonjwa wa ngiri hii ni kutokana na kuwa ubebaji wa vitu hivyo hupoteza uimara wa misuli ya tumbo.

Hayo yameelezwa na daktari bingwa wa upasuaji kutoka katika hospitali ya rufaa ya kanda Bugando Dk Ahmed Binde wakati akizungumza katika kambi maalumu ya upimaji wa magonjwa mbalimbali katika hospitali hiyo ambapo amesema ugonjwa huo hutokea pale ukuta wa tumbo unapopoteza uimara au kulegea na hii hupelekea kutengeneza uvimbe katika misuli na kwa kiasi kikubwa hali hiyo hutokea pale mtu anapokuwa anajihusisha na ubebaji wa vitu au mzigo uliyopitiliza uzito.
Dk ahmed pia amesema watu walioko hatarini kuugua ugonjwa huu ni wale wenye tatizo la tezi dume, waliofanyiwa upasuaji na wale wenye tatizo la kupata choo kwa muda mrefu na amewataka wale wanaonyanyua vyuma kufuata miongozo ya wataalamu ili kuepukana na tatizo hilo.
Kwa upande wake mkurugenzi mkuu wa hospitali hiyo Dk Fabian Massaga amesema kwa hapa nchini ugonjwa wa ngiri umeathiri asilimia 5 ya watanzania wote na kundi la wanaume ndio limeonekana kuwa na idadi kubwa ya wagonjwa wa ngiri kwani kati ya wanaume laki moja wanaume 350 wanakabiliwa na ugonjwa huo.
Dk Massaga amesema ugonjwa wa ngiri pia huathiri kundi la wanawake kwani kati ya wanawake laki moja wanawake 30 wanakadiriwa kuwa na ugonjwa huo hivyo amewataka wanawake kufanya vipimo vya ugonjwa huo ili kujua hali zao.