Kamishina wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga amezindua kampeni ya kitaifa ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia ya umeme inayokwenda na kaulimbiu ya PIKA SMART.
Mha. Luoga amezindua kampeni hiyo leo Juni 13, 2025 jijini Dar es Salaam akimwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba.

Kampeni hiyo imeandaliwa na Shirika la Modern Energy Cooking Services (MECS) chini ya ufadhili wa UKAID kwa kushirikiana na Serikali kupitia Wizara ya Nishati.
Mhandisi Luoga amesema kampeni hiyo imezinduliwa ikiwa ni mojawapo ya jitihada za Serikali kuhakikisha inawahamasisha wananchi kutumia nishati safi ya kupikia ili kufikia lengo la asilimia 80 ya watanzania kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo 2034.

Luoga amewatoa hofu wananchi kuhusu kutumia nishati safi ya kupikia ya umeme akitanabaisha kuwa ni salama na gharama nafuu na kuongeza kuwa Tanzania Ina Umeme mwingi na wa kutosheleza mahitaji.
“Kama tunavyofahamu bwawa la kufua umeme kwa maji la Julius Nyerere limekamilika na hivyo kupelekea umeme uliopo nchini hadi sasa kufikia takribani megawati 4,031, umeme huu umeshafika katika Vijiji vyote 12, 318 vya Tanzania hivyo kuna kila sababu kwa wananchi kutumia nishati safi ya umeme kupikia.” amesema Mha. Luoga.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji TANESCO, Mkurugenzi wa Mipango na uwekezaji TANESCO, Mhandisi Henryfried Byabato amesema Shirika hilo limekuwa likihamasisha wananchi kutumia nishati safi ya kupikia ya umeme kutokana na uwepo wa kutosha wa nishati hiyo nchini.
Ameongeza kuwa, teknolojia zimeboreshwa hivyo majiko ya umeme yanatumia nishati kidogo na kwa ufanisi mkubwa.

Kampeni hii ya kuhamasisha matumizi ya pika smart imekuja wakati muafaka ambapo Wizara ya Nishati imezindua mkakati wa Taifa wa Mawasiliano wenye lengo la kutoa mwongozo kwa wadau kuendeleza kampeni ya uhamasishaji matumizi ya nishati safi ya kupikia ili kuunga mkono jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Samia Suluhu Hassan ambaye ni kinara wa nishati safi ya kupikia kuhakikisha watanzania wanahama kutoka kwenye matumizi ya nishati isiyo safi kwenda kwenye nishati safi