Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani imesema imeunda kamati ya wataalam mbalimbali kuchunguza makadirio ya gharama za ujenzi wa kituo cha polisi Butiama mkoani Mara kitakachogharimu sh. Mil 802 hadi kukamilika kwake.

Akizungumza jijini Mwanza Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani Jumanne Sagini amesema kamati hiyo iliyoundwa na katibu mkuu imelenga kuangalia kama ukadiriaji wa ujenzi wa jengo upo sahihi huku pia ikiwa na lengo la kuangalia kama fedha zilizotolewa zinaenda sambamba na manunuzi ya vifaa vilivyotumika katika ujenzi huo.
Sagini pia amesema endapo kamati hiyo itabaini udanganyifu wa aina yoyote basi hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wale wote waliohusika na udanganyifu huo.
Hatua hii imekuja ikiwa ni zaidi ya wiki moja sasa mara baada ya picha za jengo hilo kusambaa katika mitandao mbalimbali ya kijamii picha zilizoibua mijadala na sintofahamu kwa wananchi wakihoji ni kwa nini kiasi cha sh. Milion 802 hakiendani na muonekano wa jengo hilo.