
Baraza la katiba la Senegal limetoa hukumu na kutangaza kwamba uamuzi uliopitishwa na bunge wa kuahirisha uchaguzi wa rais wa Februari 25 hadi Disemba haukuendana na katiba.
Kulingana na hukumu iliopitishwa na wajumbe wake saba, baraza la katiba la Senegal jana Alhamisi lilifuta amri iliyotiwa saini na rais Sall, ambayo iliahirisha uchaguzi wa rais uliokuwa umepangwa kufanyika Februari 25.
Wagombea urais wa upinzani na wabunge walikuwa wamewasilisha changamoto kadhaa za kisheria kwa mswada uliopitishwa na bunge wiki iliyopita, ambao pia ulirefusha muda wa rais Macky Sall kubaki madarakani katika kile ambacho wakosoaji wanasema ni sawa na mapinduzi ya kitaasisi.
Alipotangaza uamuzi huo katika hotuba yake kwa taifa aliyotoa Februari 3, rais Macky Sall alisema ametia saini amri ya kukomesha hatua ya awali iliyoweka tarehe hiyo, kwa sababu wabunge walikuwa wakiwachunguza majaji wawili wa baraza la katiba ambao uadilifu wao katika mchakato wa uchaguzi umetiliwa shaka.