Categories

Do you have a Story?

Call us on 0677 644 444 to submit your news story or incident report!

Dkt. Chana Apokea Tuzo Nne Za Kimataifa Za Utalii Dodoma

Na Gideon Gregory, Dodoma.

Ukuaji wa sekta ya utalii nchini imeleta mageuzi makubwa kunatokana na juhudi kubwa zinazofanywa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, jambo lililopelekea Wizara ya Maliasili na Utalii kupokea tuzo nne (4) za usafirishaji duniani kwa mwaka 2024.


Hayo yameelezwa Jijini Dodoma na Waziri wa Maliasili na Utalii Balozi Dkt. Pindi Chana wakati wa hafla ya kupokea tuzo hizo na kubainisha vipengele ambavyo wameshinda.


“Kwenye hizi tuzo tumeweza kushinda Kivutio Bora cha Utalii Afrika (African Leading Tourism Attraction 2024) – Mlima Kilimanjaro, Hifadhi Bora ya Taifa Afrika (Africa’s Leading National Park 2024) – Hifadhi ya Taifa Serengeti, Kituo Bora cha Utalii Afrika (African’s Leading Destination) – Tanzania, Bodi Bora ya Utalii Afrika (African Leading Tourism Attraction 2024) – Bodi ya Utalii Tanzania (TTB),”amesema.


Amesema Tanzania imeendelea kufanya vizuri katika kupokea watalii wa kimataifa na kuvunja rekodi zilizowekwa kabla ya kipindi cha UVIKO – 19 mwaka 2019.


“Kwa mujibu wa Ripoti ya Nusu Mwaka ya Takwimu za Utalii ya Shirika la Utalii Duniani (UN Tourism Barometer report) katika kipindi cha kuanzia mwezi Januari hadi Julai, 2024, Tanzania imeshika nafasi ya kwanza Afrika kwa nchi zilizotembelewa na idadi kubwa ya watalii wa kimataifa ikilinganishwa na mwaka 2019 kabla ya UVIKO-19,”amesema.


Sambamba na hilo ameongeza kuwa, Tanzania imepanda kutoka nafasi ya pili kwa ripoti ya kipindi kama hicho mwaka jana,na kwamba kwa rekodi hiyo Tanzania imekuwa nchi ya sita (6) duniani kwa kuwa na ongezeko la asilimia 49 la watalii ikitanguliwa na Qatar.
“Kwa takwimu hizo Tanzania imepanda hadi nafasi 2 juu ambapo kwa kipindi kama hicho, mwaka jana ilishika nafasi ya nane (8) duniani ikiwa na ongezeko la asilimia 19,”ameongeza.


Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii Dkt. Hassan Abbas amesema kupitia filamu The Royal Tour iliyoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ndiyo chachu kuu ya ushindi huo hivyo anaamini watanzania wataondokana na hofu juu ya kile walichokuwa wanahitaji kufahamu juu ya faida ya filamu hiyo.


Naye Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii Bw. Nkoba Mabula amesema tuzo hizo utolewa kila mwaka ili kutambua, kuthamini na kusherehekea ubora katika sekta ya usafiri, utalii na ukarimu duniani kote zikiwa zimeanzishwa mwaka 1993 huku zinatambulika kimataifa na kutolewa katika maeneo mbalimbali ulimwenguni.


“Washindi wa tuzo hizi huchaguliwa kupitia kura za wataalamu wa sekta na umma na ushindi unachukuliwa kuwa wa heshima kubwa na katika muktadha huo Tanzania imeendelea kushinda tuzo za World Travel Awards ambazo ni moja wapo ya tuzo kubwa na mashuhuri katika sekta ya utalii duniani, ” amesema.


Amesema katika kinyang’anyiro hicho Tanzania ilikuwa inashindanishwa na nchi nguli katika sekta ya utalii barani Afrika kama Botswana, Misri, Ghana, Kenya, Morocco, Malawi, Msumbiji, Namibia, Afrika Kusini, Nigeria, Uganda, Rwanda na Zambia na kuongeza kuwa ushindi huo unadhirisha ubora wa vivutio vilivyopo nchini.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *